Mzigo-TV-728x90

Masomo ya misa

Masomo ya Misa Machi 2

By

on

Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 02/03/2024

2024 MACHI 2 JUMAMOSI: JUMA 2 LA KWARESIMA
Mt Agnes wa Praha au Bohemia 
Urujuani
Zaburi: Juma 2

Somo 1. Mik 7: 14-15, 18-20

Walishe watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako, wakaao peke yao, mwituni katikati ya Karmeli; na walishe katika Bashani na Gileadi, kama siku za kale. Kama katika siku zile za kutoka kwako katika nchi ya Misri nitamwonyesha mambo ya ajabu. Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari. Wewe utamtimilizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.

Wimbo wa Katikati. Zab 103:1-4, 9-12

1. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana.
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

(K) Bwana amejaa huruma na neema.
  
2. Akusamehe maovu yako yote,  
Akuponya magonjwa yako yote,
Aukomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

3. Yeye hatatea siku zote,
Wala hatashika hasira yake milele.
Hakututenda sawa na hatia zetu,
Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.

4. Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)

Injili. Lk 15: 1-3, 11-32

Watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia Yesu wamsikilize. Mafarisayo na waandishi wakanung’unika, wakisema, ”Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao.” Akawaambia mfano huu, akisema, ”Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; yule mdogo akamwambia babaye, Baba, nipe sehemu ya mali inayoniangukia. Akawagawia vitu vyake. Hata baada ya siku si nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati. Alipokuwa amekwisha tumia vyote, njaa kuu iliingia nchi ile, yeye naye akaanza kuhitaji. Akaenda akashikamana na mwenyeji mmoja wa nchi ile; naye alimpeleka shambani kwake kulisha nguruwe. Akawa akitamani kujishibisha kwa maganda waliyokula nguruwe, wala hapana mtu aliyempa kitu. Alipozingatia moyoni mwake, alisema, ”Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana. Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. Lakini baba aliwaambia watumwa wake, ”Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; mleteeni ndama yule aliyenona mkamchinje; nasi tule na kufurahi; kwa kuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.” Wakaanza kushangilia. Basi, yule mwanawe mkubwa alikuwako shamba na alipokuwa akija na kuikaribia nyumba, alisikia sauti ya nyimbo na machezo. Akaita mtumshi mmoja, akamwuliza, ‘Mambo haya, maana yake nini?’ Akamwambia, ‘Ndugu yako amekuja, na baba yako amemchinja ndama aliyenona, kwa sababu amempata tena, yu mzima.’ Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi. Akamjibu baba yake, akasema. ‘Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wo wote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona. Akamwambia, ‘Mwanangu, wewe u pamoja nami sikuzote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. Tena, kufanya furaha na shangwe ilipasa, kwa kuwa huyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.”’

Tafakari

MZAZI NI MUNGU WA HAPA DUNIANI: Kuna usemi wa wahenga usemao “Damu ni nzito kuliko maji.” Maana halisi ya usemi huu ni kuwa, ndugu wa damu ana umuhimu wa kipekee, hata akifanya kosa laweza angaliwa kwa namna tofauti na inavyotarajiwa. Huyu baba tuliyemsikia katika Injili, kitendo alichokifanya cha kumpokea mwanae huyu aliyekwisha tapanya mali yake kwa ulevi na maisha ya kihuni, na sasa anarudi tena nyumbani. Kwa ulimwengu wa leo hii ni vigumu sana, sio ajabu kwa wengine wetu tungemfukuza au kumfungulia mashtaka ya wizi au ubadhirifu wa mali na hata tukasahau kuwa ni ndugu. Baba huyu anasimama katika nafasi ya Mungu, kuwa Mungu anatuhurumia na kutusamehe bila hata kujali uzito wa kosa ili mradi mhusika/mdhambi amechukua hatua na kurudi kwa unyenyekevu na kukiri kosa/dhambi husika wazi wazi. Leo hii tujiulize tunaungamaje dhambi zetu? Je tunazitaja wazi wazi na kukusudia kuziacha? Au tunaungama kwa kuficha nyingine kwa kusema, ‘naungama na zile nilizozisahau’ angali unazikumbuka vyema, au tunaona aibu kuungama!

SALA: Baba wa Huruma, tunaomba neema ya kutambua makosa yetu na kuyakiri bila kificho kwako.

About mzigotv

Nyimbo Mpya 2023, 2022 Download Audio, Video, Mp3, Mp3 African music, Tanzania Music, Naijamusic, naijavibe, Bekaboy, Djmwanga, Tanzania songs, Kenya songs, Uganda songs, Rwanda songs, Congo songs, Zanzibar, Singeli, Taarabu, Reggae, Amapiano, Nyimbo za dini, Gospel songs, Diamond platnumz, jux, Rayvanny, Harmonize, Nandy, Zuchu, Wasafi, Alikiba Teading songs, Top 100 songs youtube, Nigeria, Naija songs.

Recommended for you