
Tumsifu Yesu Kristu… Karibu Katika Masomo ya Misa Takatifu 29/02/2024
2024 FEBRUARI 29 ALHAMIS: JUMA 2 LA KWARESIMA
Mt. Aswoldi, Askofu
Urujuani
Zaburi: Juma 2
Somo 1. Yer 17: 5-10
Bwana asema hivi: ”Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, hataona yatakapotokea mema; bali atakaa jangwani palipo ukame, katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bichi; wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaacha kuzaa matunda. Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.
Wimbo wa Katikati Zab 1:1-4, 6
1. Heri mtu Yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sharia ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku . (K)
(K) Heri aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake.
2. Naye atakuwa kama mti uliopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K)
3. Sivyo walivyo wasio haki;
Hao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.
Kwa kuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea. (K)
Injili. Lk 16: 19-31
Yesu aliwaambia Mafarisayo: ”Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamlamba vidonda vyake. Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa. Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake. Akalia, akasema, ”Ee baba Ibrahimu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu. Ibrahimu akasema, ‘Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu’. Akasema, ‘Basi, baba, nakuomba, umtume nyumbani kwa baba yangu, kwa kuwa ninao ndugu watano, ili awashuhudie, wasije wao pia wakafika mahali hapa pa mateso’. Ibrahimu akasema, ‘Wanao Musa na manabii; na wawasikilize wao.’ Akasema, ‘La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea mtu atokaye kwa wafu, watatubu.’ Akamwambia, ‘Wasipowasikia Musa na manabii, hawatashawishiwa hata mtu akifufuka katika wafu.”’
TAFAKARI
MAMBO YA DUNIANI NI YA MUDA MFUPI, YADUMUYO NI YA MBINGUNI: Licha yetu sisi wanadamu kuwa na akili na utashi, bado tunaangukia katika wimbi la kutopambanua na kuchagua vema. Wengi tunachagua mambo yatuleteayo vionjo vya kidunia na si wokovu wetu. Wengi tunajiamini na kuwaamini wanadamu wenzetu na si Mungu. Tumeshuhudiwa na ujumbe wa Bwana uelezao juu ya kulaaniwa mtu amtegemeaye mwanadamu na kubarikiwa mtu amtegemeaye Bwana. Namna hii ya uovu tunaiona kwa tajiri ambaye amekuwa akilimbikiza mali na kutomjali Lazaro aliyekuwa maskini. Baada ya vifo vyao Lazaro anafurahia na malaika mbinguni, lakini tajiri anateseka kuzimu. Tajiri alijikita katika kujilimbikizia mali za ulimwengu huu zipitazo lakini Lazaro alijitafutia mbingu angali hapa duniani. Katika maisha yetu tuwe watu wa kujali wenzetu, watu wa majitoleo tuwasaidie wenzetu tungali bado hapa dunia hasa kuwaelekeza kumfahamu na kumtegemea Mungu. Wakati wetu ni sasa tusisubiri baadaye. Yote tuyatende kwa sifa na utukufu wa Mungu na si kwa kujionesha mbele ya wanadamu.
SALA: Tunakuomba Mwenyezi Mungu utukuwa chachu ya kuwajali wenzetu na tuyafanye yote kwa sifa na utukufu wako. Amina.
