Masomo ya misa

Masomo ya Misa Oktoba 9

By

on

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 09/10/2024

2024 OKTOBA 9: JUMATANO-JUMA LA 27 LA MWAKA

Mt. Dionisi, Askofu na Wenzake, Mashahidi/ Mt. Yohane Leonardi, Padre
Rangi:Kijani

Zaburi: Juma III

SOMO 1. Gal 2:1-2, 7-14

Baada ya miaka kumi na minne, nalipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua na Tito pamoja nami. Nami nalikwenda kwa kuwa nalifunuliwa, nikawaeleza injili ile niihubiriyo katika Mataifa, lakini kwa faragha kwa hao walio wenye sifa, isiwe labda napiga mbio bure, au nalipiga mbio bure. Bali, kinyume cha nayo, walipoona ya kuwa nimekabidhiwa injili ya wasiotahiriwa, kama vile Petro ya waliotahiriwa. Maana yeye aliyemwezesha Petro kuwa mtume wa waliotahiriwa ndiye aliyeniwezesha mimi kwenda kwa mataifa. Tena walipokwisha kuijua ile neema niliyopewa; Yakobo, na Kefa, na Yohane, wenye sifa kuwa ni nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika; ili sisi tuende kwa mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara; ila neno moja tu walitutakia, tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii kulifanya. Lakini Kefa alipokuja Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu. Kwa maana kabla hawajaja watu kadha wa kadha waliotoka kwa Yakobo, alikuwa akila pamoja na watu wa Mataifa; lakini walipokuja wao, akarudi nyuma akajitenga, huku akiwaogopa waliotahiriwa. Na hao Wayahudi wengine wakajigeuza pamoja naye, hata Barnaba pia akachukuliwa na unafiki wao. Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, “Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha mataifa kufuata desturi za Wayahudi?

WIMBO WA KATIKATI. Zab 117

1. Aleluya.
Enyi mataifa yote, msifuni Bwana,
Enyi watu wote, mhimidini.

(K) “Enendeni ulimwenguni wote,
mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. “

2. Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu,
Na uaminifu wa Bwana ni wa milele. (K)

INJILI. Lk 11:1-4

Yesu alipokuwa mahali fulani akiomba, alipokwisha, mmoja katika wanafunzi wake alimwambia, “Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile Yohane alivyowafundisha wanafunzi wake.” Akawaambia, “Msalipo, semeni: Baba, Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, Utupe siku kwa siku riziki yetu. Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni.”

TAFAKARI.

JIFUNZE KUSALI NA KUSAMEHE: Inaonekana maisha ya sala ni rahisi sana. Unatafuta mahali pa ukimya, kisha unazungumza na Mungu. Lakini hata wafuasi wa Yesu waliomba kufundishwa kusali, hili likionesha kwamba, hawakuwa na ufahamu wa kutosha katika sala na kwa sababu hiyo walihitaji elimu hiyo. Mara ya mwisho ni lini ulijifunza kusali? Makundi mbali mbali wanalisaidia Kanisa na kuwaongoza watu kujua nini maana ya sala. Nawe fanya hivyo; elekeza, wasiliana na watu na anzisha vikundi vidogo vidogo vya sala ukianzia katika familia. Kuhusu msamaha; kuwasamehe wale waliotukosea ni jambo gumu sana. Frank amenisaliti, John ameniibia, na Richard amenidanganya. Kuwasamehe watu hawa ni ngumu sana. Lakini hata hivyo Kristo anatualika kuwasamehe. Hivi ndivyo unavyoweza kuanza kuwa mtu wa msamaha: Fikiria jinsi ulivyozishika amri za Mungu kwa kiwango cha chini kabisa. Kusudi Mungu aweze kukusamehe, unahitajika upendo mkubwa sana. Kumbuka watu wanaoweka kisasi jinsi walivyo. Sala zetu zituongeze katika kusameheana. 

SALA: Bwana utujalie moyo wa sala na majuto pale tunapokosea nasi tukumbuke kuwasamehe waliotukosea.

About mzigotv

Nyimbo Mpya 2025 2024 2023 2022 Download Audio, Video, Mp3, Mp3 African music, Tanzania Music, Naijamusic, naijavibe, Bekaboy, Djmwanga, Tanzania songs, Kenya songs, Uganda songs, Rwanda songs, Congo songs, Zanzibar, Singeli, Taarabu, Reggae, Amapiano, Nyimbo za dini, Gospel songs, Diamond platnumz, jux, Rayvanny, Harmonize, Nandy, Zuchu, Wasafi, Alikiba Teading songs, Top 100 songs youtube, Nigeria, Naija songs.

Recommended for you