Mzigo-TV-728x90

Masomo ya misa

Masomo ya Misa Mei 7

By

on

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 07/05/2024

2024 MEI 7 : JUMANNE-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Rose Venerini
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 2

Somo 1. Mdo 16:22-34

Siku ile pale Filipi, wenyeji waliwakamata Paulo na Sila, wakawaendea, makadhi wakawavua nguo zao kwa nguvu, wakatoa amri wapigwe kwa bakora. Na walipokwisha kuwapiga mapigo mengi, wakawatupa gerezani, wakamwamuru mlinzi wa gereza awalinde sana. Naye akiisha kupata amri hii akawatupa katika chumba cha ndani, akawafunga miguu kwa mkatale. Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu, akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. Akataka taa ziletwe, akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako. Wakamwambia neno la Bwana, yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake.  Akawakaribisha saa ile ile ya usiku, akawaosha mapigo yao, kisha akabatizwa, yeye na watu wake wote wakati huo huo. Akawaleta juu nyumbani kwake, akawaandalia chakula, akafurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana amekwisha kumwamini Mungu.

Wimbo wa Katikati. Zab 138:1-3, 7-8

1. Nitakushukuru kwa moyo wangu wote,
Mbele ya miungu nitakuimbia zaburi.
Nitasujudu nikilikabili hekalu lako takatifu. 

(K) Utanyosha mkono, Ee Bwana, utaniokoa.

2. Kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako,
Kwa maana umeikuza ahadi yako,
Siku ile niliyokuita uliniitikia,
Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu. (K)

3. Utanyosha mkono juu ya hasira ya adui zangu,
Na mkono wako wa kuume utaniokoa.
Ee Bwana, fadhili zako ni za milele;
Usiziache kazi za mikono yako. (K)

Injili. Yn 16:5-11

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake:  Sasa mimi naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka, wala hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?  Ila kwa sababu nimewaambia hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu. Lakini mimi  nawambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke; kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu. Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena; kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa.

TAFAKARI

ROHO MTAKATIFU NI MSAIDIZI WETU: Katika Injili ya leo tumemsikia Yesu akiwaaga wanafunzi wake kuwa anarudi kwa yule aliyemtuma. Kama ilivyo kawaida kwa watu waliozoeana kwa muda mrefu kuagana, ndivyo ilivyokuwa kwa wafuasi wa Kristo. Wamehuzunika kwasababu wanalazimika kuagana na Kristo japo hawapendi. Huzuni yao ilisukumwa na ukweli kwamba watakosa uwepo wa Yesu kati yao kwa muda. Yesu anatuliza huzuni yao kwa kuwahakikishia kuwa atampeleka Roho Mtakatifu. Yesu anawaeleza kuwa Roho Mtakatifu atakapokuja atawafumbulia mambo mengi ikiwemo kuudhihirishia ulimwengu kuwa ulianguka katika dhambi ya kutomwamini Mwana wa Mungu. Tunaalikwa tutambue nafasi ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu. Katika kupokea Sakramenti ya upatanisho Roho Mtakatifu ni muhimu kwani anatukumbusha ni wapi tumekosea na hivyo tufanye toba ya kweli na kujirudi. Tumruhusu Roho Mtakatifu atuangaze katika maisha yetu.

SALA: Ewe Roho Mtakatifu uje ukawe Msaidizi wetu katika utume wetu.

About mzigotv

Nyimbo Mpya 2023, 2022 Download Audio, Video, Mp3, Mp3 African music, Tanzania Music, Naijamusic, naijavibe, Bekaboy, Djmwanga, Tanzania songs, Kenya songs, Uganda songs, Rwanda songs, Congo songs, Zanzibar, Singeli, Taarabu, Reggae, Amapiano, Nyimbo za dini, Gospel songs, Diamond platnumz, jux, Rayvanny, Harmonize, Nandy, Zuchu, Wasafi, Alikiba Teading songs, Top 100 songs youtube, Nigeria, Naija songs.

Recommended for you