Mzigo-TV-728x90

Masomo ya misa

Masomo ya Misa Mei 4

By

on

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 04/05/2024

2024 MEI 4 : JUMAMOSI-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Godehardi, Askofu”
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Mdo 16:1-10

Siku zile, Paulo alifika Derbe na Listra na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vyema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio. Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtairi kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani. Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku. Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. Walipofika kukabili Misia, wakajaribu kwenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, wakapita Misia wakatelemka Troa. Paulo akatokewa na maono usiku; alimwona mtu wa Makedonia amesimama, akimsihi, na kumwambia, vuka, uje Makedonia utusaidie. Basi alipokwisha kuyaona yale maono, mara tukataka kutoka kwenda Makedonia, kwa kuwa tuliona hakika ya kwamba Mungu ametuita tuwahubiri Habari Njema.

Wimbo wa Katikati. Zab 100:1-3, 5

“1. Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote
Mtumikieni Bwana kwa furaha.
Njoni mbele zake kwa kuimba; (K)

K) Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote.

2. Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu;
Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake;
Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)

3. Kwa kuwa Bwana ndiye mwema;
Rehema zake ni za milele;
Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)”

Injili. Yn 15:18-21

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.

TAFAKARI

ULIMCHUKIA KRISTO, UTATUCHUKIA NA SISI PIA: Tupo ulimwenguni lakini hatupaswi kuwa wa ulimwengu. Kwa ubatizo wetu tumechaguliwa na Yesu tusiwe tena wa ulimwengu. Matendo yetu, maneno yetu, na namna yetu ya kuishi, havipaswi kufuata mawimbi ya ulimwengu huu. Tunapaswa kuwa mwanga pale ulimwengu unapokuwa giza, tunapaswa kuleta ladha ulimwenguni pale ulimwengu unapopoteza ladha. Haya yote ni kwenda kinyume na mkondo wa walimwengu wa sasa, na hivyo tukiendelea hivyo tuwe tayari kuchukiwa kwa matendo yetu yasiyoendana na ya walimwengu kwani matendo yetu yanapaswa kuwashitaki walimwengu. Tusife moyo kwani tunachota nguvu kutoka kwa Yesu kwani kama ulimwengu ulivyomchukia Kristo, utatuchukia sisi wafuasi wake pia. Watakatifu wengi walikubali kwenda kinyume na ulimwengu na malimwengu hata wakamwaga damu yao kwa ajili ya Kristo. Mtakatifu Karoli Lwanga na wenzake ni kielelezo hapa kwetu Afrika Mashariki jinsi walivyokubali kufa wakiishuhudia imani.

SALA: Ee Yesu nijalie uvumilivu katika magumu yaletwayo na Maisha ya ufuasi.

About mzigotv

Nyimbo Mpya 2023, 2022 Download Audio, Video, Mp3, Mp3 African music, Tanzania Music, Naijamusic, naijavibe, Bekaboy, Djmwanga, Tanzania songs, Kenya songs, Uganda songs, Rwanda songs, Congo songs, Zanzibar, Singeli, Taarabu, Reggae, Amapiano, Nyimbo za dini, Gospel songs, Diamond platnumz, jux, Rayvanny, Harmonize, Nandy, Zuchu, Wasafi, Alikiba Teading songs, Top 100 songs youtube, Nigeria, Naija songs.

Recommended for you